DKT. MIGIRO NI CHACHU YA MATUMAINI MAKUBWA KWA VIONGOZI WA MASHINA – MWENEZI KENANI
07 Jan, 2026
70 Machapisho
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa anayeshughulikia Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Kihongosi, amesema Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Balozi Dkt. Asha Rose Migiro, ni chachu ya matumaini makubwa kwa viongozi wa mashina na wanachama wa chama hicho kutokana na uongozi wake wa mfano, unaojikita katika kulea, kufundisha na kuwaimarisha viongozi kuanzia ngazi ya chini.
Akizungumza leo, tarehe 7 Januari 2026, jijini Dar es Salaam wakati wa kuanza kwa ziara ya Katibu Mkuu Dkt. Migiro ya kukutana na kuzungumza na mabalozi wa mashina kutoka Wilaya za Temeke na Kigamboni, Mwenezi Kenani ametoa pongezi zake za dhati kwa Katibu Mkuu huyo kwa kuendelea kuwa mlezi na mwalimu bora wa viongozi na wanachama wa CCM.
Amesema kuwa uongozi wa Dkt. Migiro umejengwa juu ya misingi ya malezi, mafunzo na maadili, jambo linalowafanya wanachama wa CCM kujivunia uwepo wake. Katika maelezo yake, Mwenezi Kenani amesema:
“Katibu Mkuu wetu Dkt. Migiro ni kiongozi wa mfano. Umetulea vema, umetufundisha, na pale tunapokosea umekuwa mama mlezi wetu. Tunajivunia kuwa sehemu ya uongozi wako kwa sababu umeendelea kuwa mwalimu bora ndani ya Chama Cha Mapinduzi.”
Aidha, Mwenezi Kenani amepongeza kauli mbiu ya Katibu Mkuu kwa mabalozi wa mashina isemayo ‘Shina Lako Linakuita’, akieleza kuwa kauli hiyo imekuja kwa wakati muafaka na inalenga kuamsha uhai mpya wa chama kuanzia ngazi ya shina, ambayo ndiyo msingi na nguzo kuu ya CCM.
Amesisitiza kuwa msisitizo wa kushuka chini na kutembelea mashina unaonesha dhamira ya dhati ya Katibu Mkuu ya kufanya mageuzi chanya ndani ya CCM na jumuiya zake, akibainisha kuwa hilo ni jambo la heshima kubwa kwa viongozi wa mashina na mabalozi wao.
“Kauli mbiu hii ya ‘Shina Lako Linakuita’ inathibitisha dhamira yako ya kufanya mageuzi makubwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi. Mashina ndiyo mali, msingi na nguzo ya CCM, na kuyatambua na kuyapa heshima ni kulijenga chama kwa misingi imara,” ameongeza.
Katika hatua nyingine, Mwenezi Kenani amewahimiza Watanzania wote kuendelea kuilinda amani ya Taifa kwa wivu mkubwa, akisisitiza kuwa amani hiyo ndiyo msingi wa maendeleo endelevu. Ameongeza kuwa Tanzania imebahatika kuwa na Rais Mwanamama mwenye upendo, busara na dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi na kuendelea kuleta maendeleo kwa Taifa kwa ujumla.
Ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Asha Rose Migiro, jijini Dar es Salaam inaendelea kuonekana kama jukwaa muhimu la kuimarisha mshikamano wa chama, kuwasikiliza mabalozi wa mashina na kujenga dira mpya ya utendaji inayolenga kuimarisha CCM kuanzia ngazi ya chini kabisa.
Habari Zinazohusiana
KATIBU MKUU WA UVCCM KUONGOZA KIKAO CHA SEKRETARIETI YA BARAZA KUU LA UVCCM, ZANZIBAR
09 Feb, 2026
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Ndugu Halid Mwinyi (MNEC), anatarajiwa kuongoza kikao cha Sekretarieti ya Baraza Kuu la UVCCM kitakachofanyika Jumanne, tarehe 10 Februari 2026, katika Chuo cha Umoja wa Vijana Tunguu, Zanzibar.
RAIS DKT. SAMIA AZINDUA SOKO JIPYA LA KARIAKOO: AFUNGUA UKURASA MPYA WA TUMAINI LA KIUCHUMI, AAGIZA HAKI, UWAZI NA USALAMA KWA WAFANYABIASHARA
08 Feb, 2026
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amezindua rasmi Jengo Jipya la Soko la Kariakoo
RAIS DKT. SAMIA AAGIZA UTUNZAJI WA MIUNDOMBINU, UJENZI WA KITUO CHA WATOTO NA ELIMU YA ZIMAMOTO SOKO JIPYA LA KARIAKOO
08 Feb, 2026
Dar es Salaam 08 Februari 2026 Katika kulinda uwekezaji wa umma na kuhakikisha thamani ya fedha za wananchi inalindwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu wa kutunza na kusimamia miundombinu ya Soko