INJINI YA CCM IPO MASHINANI; DKT. MIGIRO ASISITIZA UONGOZI WA KARIBU NA WANANCHI
13 Jan, 2026
43 Machapisho
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amesema kuwa mashina ndiyo injini halisi ya uhai, uhalali na maendeleo ya Chama Cha Mapinduzi, akisisitiza kuwa maendeleo ya kweli ya wananchi huanzia katika ngazi za chini za chama.
Dkt. Migiro ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na Mabalozi wa Mashina wa CCM Wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam, katika mkutano uliokuwa ni hitimisho la ziara yake ya kuimarisha chama Mkoa wa Dar es Salaam, chini ya kaulimbiu “Shina Lako Linakuita”.
Akizungumza katika mkutano huo, Dkt. Migiro amesema mashina ndiyo ngazi ya kwanza inayowaunganisha wananchi moja kwa moja na Chama, kwani ndiko wanakotoka wananchi wenyewe na ndiko changamoto zao halisi zinapojadiliwa, kusikilizwa na kufanyiwa kazi.
Amesisitiza kuwa uhalali wa uongozi wa CCM unaonekana wazi kupitia ukaribu wake na wananchi katika mashina, hivyo viongozi wa ngazi za Mashina, Matawi na Kata wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha wanakuwa macho, wasikivu na wanashiriki kikamilifu katika kusimamia na kunufaika na maendeleo yanayotekelezwa ndani ya chama na serikalini.
Dkt. Migiro ameongeza kuwa maendeleo ya kisiasa na maendeleo ya kijamii hayawezi kutenganishwa, akieleza kuwa mashina imara huwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji, jambo linaloongeza imani ya wananchi kwa Chama Cha Mapinduzi.
Aidha, amewataka Mabalozi wa Mashina kuendelea kupandisha na kulinda bendera ya chama katika maeneo yao, kwa kuwa wao ni mabalozi wa kwanza wa sera, maadili na mwelekeo wa CCM katika jamii.
Katibu Mkuu huyo ameweka bayana kuwa CCM imejengwa juu ya misingi ya umoja wa kitaifa, kwa kuwashirikisha Wanachama na wasio Wanachama katika shughuli za maendeleo, bila kujali tofauti za kikanda, kijamii au kiitikadi.
Katika hatua nyingine, Dkt. Migiro amesema Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongeza kazi kubwa inayofanywa na Mabalozi wa Mashina nchi nzima, akisisitiza kuwa chama kitaendelea kuwajali, kuwathamini na kuwaunga mkono, kutokana na mchango wao mkubwa katika kuimarisha chama kuanzia ngazi ya chini kabisa.
Amehitimisha kwa kusisitiza kuwa nguvu ya CCM iko kwa wananchi, na wananchi hao wanapatikana mashinani, hivyo kuimarisha mashina ni kuimarisha chama na mustakabali wa maendeleo ya Taifa.
#ShinaLakoLinakuita
Habari Zinazohusiana
KATIBU MKUU WA UVCCM KUONGOZA KIKAO CHA SEKRETARIETI YA BARAZA KUU LA UVCCM, ZANZIBAR
09 Feb, 2026
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Ndugu Halid Mwinyi (MNEC), anatarajiwa kuongoza kikao cha Sekretarieti ya Baraza Kuu la UVCCM kitakachofanyika Jumanne, tarehe 10 Februari 2026, katika Chuo cha Umoja wa Vijana Tunguu, Zanzibar.
RAIS DKT. SAMIA AZINDUA SOKO JIPYA LA KARIAKOO: AFUNGUA UKURASA MPYA WA TUMAINI LA KIUCHUMI, AAGIZA HAKI, UWAZI NA USALAMA KWA WAFANYABIASHARA
08 Feb, 2026
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amezindua rasmi Jengo Jipya la Soko la Kariakoo
RAIS DKT. SAMIA AAGIZA UTUNZAJI WA MIUNDOMBINU, UJENZI WA KITUO CHA WATOTO NA ELIMU YA ZIMAMOTO SOKO JIPYA LA KARIAKOO
08 Feb, 2026
Dar es Salaam 08 Februari 2026 Katika kulinda uwekezaji wa umma na kuhakikisha thamani ya fedha za wananchi inalindwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu wa kutunza na kusimamia miundombinu ya Soko